1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahamiaji wanaotafuta ajira waongezeka Ulaya Mashariki

24 Julai 2023

Licha ya mataifa ya Poland na Hungary kupinga mpango wa Umoja wa Ulaya wa kugawana wahamiaji, kumeshuhudiwa ongezeko la wahamiaji wanaowasili katika nchi za mashariki mwa Ulaya kwa lengo la kutafuta ajira.

https://p.dw.com/p/4UJOc
Türkische Gastarbeiter im BMW-Motorradwerk - Entwicklung der Migration nach Deutschland Flash-Galerie
Picha: picture alliance/dpa

Kumeshuhudiwa mabadiliko makubwa nchini Poland na katika nchi nyingine za Ulaya ya Kati na Mashariki (CEE. Nchi nyingi wanachama wa Umoja wa Ulaya (EU) katika eneo ambalo hapo zamani lilitawaliwa na ukomunisti, zimebadili kwa kasi ya ajabu hadhi yao kutoka kwenye mataifa yenye soko inayoendelea hadi kufikia hali ya soko iliyoendelea katika muda wa miaka 19 tu tangu kujiunga kwao na Umoja wa Ulaya.

Soma pia: Meloni: Tushirikiane kudhibiti wimbi la wahamiaji Ulaya

Hali hii bila shaka iliwezesha uwekezaji mkubwa, lakini pia baadhi ya adha za uchumi wa Magharibi ambazo ni idadi kubwa ya wazee, uhaba wa wafanyakazi, mishahara inayoongezeka kwa kasi na hitaji la uhamiaji kwa lengo la kuwavuta wafanyakazi. Uhaba huo ni mkubwa zaidi katika sekta za kiuchumi kama vile viwanda, taaluma ya afya, usafirishaji na teknolojia ya habari (IT).

Historia ya mabadiliko ya demografia

Ungarn/Serbien tschechische und slowakische Polizisten schützen gemeinsam die Grenze
Eneo la mpaka kati ya Hungary na SerbiaPicha: imago images/CTK Photo

Uhaba huo wa wafanyakazi katika mataifa ya mashariki mwa Ulaya ni matokeo ya mabadiliko ya demografia hasa kutokana na idadi ya watu wanaozeeka, uhamiaji pamoja na ukuaji mkubwa wa uchumi.

Nchi nyingi katika eneo hilo zilikumbwa na tatizo la kupungua kwa idadi ya watu katika kipindi cha miaka 15 iliyopita. Data za shirika la Huduma za Ajira barani Ulaya  (EURES), ambao ni mtandao unaolenga kuwezesha mpango mzima wa wafanyakazi kusafiri kwa uhuru katika Umoja wa Ulaya, linaonyesha kuwa karibu nchi zote za Ulaya ya Kati na Mashariki (CEE) zilikabiliwa na tatizo la kupungua kwa idadi ya watu kati ya mwaka 2010 na 2021.

Idadi ya watu wenye umri wa kufanya kazi (ambao ni kuanzia miaka 20-64) katika nchi za eneo la CEE inatarajiwa kupungua kwa takriban 30% ifikapo mwaka 2050, na hii ni kutokana na uhamiaji na viwango vya chini vya watoto wanaozaliwa.

Soma pia: Italia na Poland zataka ufumbuzi wa mzozo wa wahamiaji

Katika muongo uliopita, pengo kati ya idadi ya watu wenye umri usiowaruhusu kufanya kazi na idadi ya watu walio na umri wa kufanya kazi limeongezeka. Kulingana na ofisi ya ustawi wa jamii ya Poland (ZUS), ili kuziba pengo hilo, idadi ya wahamiaji walio katika umri wa kufanya kazi inatakiwa kuongezeka kila mwaka hadi kufikia watu 200,000 hadi 400,000 nchini Poland pekee.

Mpito kuelekea nishati safi waunda upya soko la ajira

Nadia Kurtieva, mtaalam katika Shirikisho la biashara la Poland (Lewiatan) ameiambia DW kuwa muktadha wa mpito kuelekea nishati safi inayozoeleka kama mabadiliko ya kijani pamoja na yale ya kidijitali lazima vizingatiwe kwa kuwa vinaunda upya soko la ajira kwa kuzalisha fursa mpya za kazi na kushawishi aina za ujuzi na utaalamu ambao makampuni na mashirika yanahitaji.

Ukraine | Ukraine Krise | Menschen auf dem Weg zur ungarischen Grenze
Wakimbizi kutoka Ukraine wakiingia Hungary mwezi Februari,2022Picha: Janos Kummer/Getty Images

Baadhi ya nchi za CEE pia zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa wafanyakazi wenye ujuzi katika soko lao la ndani kutokana na raia wao pia kuondoka katika mataifa hayo hasa katika taaluma ambazo ni nadra na muhimu.

Soma zaidi: Kuna ongezeko la wahamiaji haramu Ulaya 2022

Kulingana na Benki ya Dunia, Slovenia ilikuwa na idadi kubwa zaidi ya wahamaji katika nchi za CEE, ikiwa na idadi ya watu 4,568 mnamo mwaka 2021. Uhamiaji halisi ni uwiano wa kila mwaka unaozingatia uhamiaji na pia raia wanaoihama nchi yao. Romania ilikabiliwa zaidi na tatizo hilo ambapo raia wake wapatao 12,724 waliondoka.

Hali hii imebadilika kufuatia uvamizi wa Urusi nchini Ukraine, ambao umekuwa na athari kubwa katika mahitaji ya wafanyakazi katika eneo hilo. Hivi sasa, Poland inawahifadhi idadi kubwa zaidi ya wakimbizi kutoka Ukraine ambao wanakadiriwa kufikia milioni 1.