1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAzerbaijan

Azerbaijan yaialika Armenia kwa mazungumzo ya amani

Tatu Karema
21 Novemba 2023

Wizara ya mambo ya nje ya Azerbaijan imeialika Armenia kushiriki katika mazungumzo ya mchakato wa amani. Mshauri wa Rais wa Azerbaijan Hikmet Hajiyev amesema nchi hizo hazihitaji muingilio wa Mataifa ya Magaharibi

https://p.dw.com/p/4ZGJn
Rais wa Azerbaijan Ilham Aliyev akitoa hotuba katika kongamano moja mjini Baku mnamo Oktoba 2, 2023
Rais wa Azerbaijan - Ilham AliyevPicha: Azerbaijani Presidency/AA/picture alliance

Hajiyev ameliambia shirika la habari la Reuters kwamba makubaliano ya amani sio fizikia ya nyuklia na kwamba kama kuna nia njema, kanuni za msingi za makubaliano ya amani zinaweza kufikiwa katika kipindi cha muda mfupi. Lakini kuhusiana na suala la kuhusika kwa mataifa ya Magharibi, amesema kuwa wanahitaji amani katika kanda hiyo na wala sio Marekani, Paris ama Ubelgiji.

Armenia yaupongeza Umoja wa Ulaya kwa juhudi za amani

Wiki hii, waziri mkuu wa Armenia Nikol Pashinyan aliupongeza Umoja wa Ulaya kwa kusaidia kuleta karibu makubaliano ya amani, lakini akasema pande hizo mbili bado zinazungumza lugha tofauti za kidiplomasia.

Soma pia: Armenia na Azerbaijan zakubaliana msingi wa mkataba wa amani

Hajiyev amesema Marekani imeonesha upendeleo na mtazamo usiokuwa na tija. Azerbaijan pia imeikosoa pakubwa Ufaransa ambayo mwezi uliopita ilikubali mikataba mipya ya kusambaza vifaa vya kijeshi kwa Armenia.

Azerbaijan yaishtumu Ufaransa kwa kuvuruga uthabiti

Katika hotuba kwa kongamano moja leo kuhusu kuondoa ukoloni, rais wa Azerbaijan Ilham Aliyev, alisema kuwa Ufaransa inahusika na uhalifu mwingi wa umwagaji damu katika historia ya ukoloni wa ubinadamu.

Shambulizi la kijeshi katika eneo la Nagorno Karabakh mnamo Oktoba 7, 2020
Shambulizi la kijeshi katika eneo la Nagorno KarabakhPicha: Reuters

Aliyev pia amesema kuwa Ufaransa inavuruga uthabiti sio tu katika makoloni yake ya zamani na ya sasa, lakini pia katika eneo zima la Caucasia lililo na maeneo ya nchi za Georgia, Armenia na Azerbaijan, ambapo inaunga mkono mwelekeo wa kujitenga na wanaotaka kujitenga.

Marekani kutoa msaada zaidi kwa Nagorno Karabakh

Katika hatua nyingine, Marekani itatoa  msaada wa zaidi ya dola milioni 4.1 kwa watu walioathirika na ghasia katika eneo la Nagorno-Karabakh. Haya ni kulingana na taarifa ya Shirika la Marekani kwa Maendeleo ya Kimataifa USAID  baada ya hatua ya Azerbaijan ya kulikomboa eneo hilo kusababisha kuhama kwa Waarmenia wengi.

USAID imesema kuwa msaada wa ziada ambao haukuripotiwa awali, utasaidia juhudi za kutoa msaada kwa takriban wakimbizi 74,000 na watu wa eneo hilo waliopoteza makazi waliokimbilia hifadhi nchini Armenia.

Soma pia:Waziri mkuu wa Armenia asema mipango ya mkutano na rais wa Azerbaijan yaendelea

Msaada huo utaongeza chakula cha msaada na ulinzi wa kibinadamu pamoja na makazi ya dharura.

Kulingana na taarifa hiyo, msaada huo wa ziada utafikisha msaada jumla wa kibinadamu wa Marekani katika eneo la Karabakh kufikia takriban dola milioni 28 tangu mwaka 2020.

Taarifa hiyo imeendelea kusema kuwa Marekani inasimama na raia walioathirika kutokana na oepresheni za kijeshi za Azerbaijan na kuunga mkono juhudi za serikali ya Armenia kuwasaidia wanaohitaji msaada.